.

.

09 Julai 2015

RAIS KIKWETE AHUTUBIA BUNGE LA KUMI NA LA MWISHO KATIKA UONGOZI WAKE

Rais Jakaya Kikwete amelihutubia bunge la kumi na la mwisho kwa uongozi wake ambapo ameainisha mafanikio ambayo yamepatikana tangu aingie madarakani ikiwemo kupunguza matukio ya uhalifu na ujambazi na kuongeza kuwa changamoto kubwa inayoikabili taifa hivi sasa ni tatizo la ajali za barabarani.
Viongozi mbalimbali wa serikali, marais na mawaziri wakuu wastaafu pamoja na mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao hapa nchini wamefika bungeni mjini hapa na kushiriki kusikiliza hotuba ya rais ambapo mara baada ya rais Kikwete kuwasili viwanja vya bunge wimbo wa taifa uliimbwa na baadae akakagua gwaride liloandaliwa maalum kwa shughuli hiyo.

Katika hotuba yake rais Kikwete mbali na kuwashukuru wabunge kwa ushirikiano waliompa na kazi kubwa walizofanya za kupitisha miswada mbalimbali ya sheria amesema nchi iko salama na kuwahakikishia watanzania kuwa atahakikisha anaiacha salama na kwamba serikali yake itaendelea kutatua changamoto zilizopo hivi sasa kwa kipindi kilichobaki ikiwemo msongamano wa wafungwa magerezani.

Awali kabla ya rais Kikwete kuhutubia bunge waziri mkuu Mh Mizengo Pinda alihitimisha rasmi mkutano wa ishirini wa bunge huku akitangaza wilaya mpya sita ikiwemo wilaya ya Ubungo na wilaya ya Kigamboni kwa jiji la Dar es Salaam na akatumia nafasi hiyo kuwaaga na kuwashukuru wabunge kwa ushirikiano waliompa katika kipindi chote tangu alipoteuliwa kushika wadhifa huo.

Kwa upande wake spika wa bunge Mh Anne Makinda amewataka watanzania kuimarisha tabia nzuri na amani iliyopo nchini na waache chokochoko za hapa na pale hasa tatizo la kuumizana lililoanza kujitokeza ambapo baadhi ya watu wameumizwa wakati wa zoezi la kuandikishwa kwenye daftari la kudumu la wapiga kura.

Tofauti na maudhurio ya vikao vya bunge vilivyokuwa vinaendelea hapa bungeni idadi ya wabunge imeongezeka mara dufu wakati wa hotuba ya rais licha ya wabunge wa kambi ya upinzani bungeni kutokuwepo.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni