.

.

04 Aprili 2016

TAARIFA KWA UMMA,MAMLAKA YA MAPATO TANZANIA[TRA]IMEKUSANYA MAPATO MWEZI MACHI 2016 KWA ASILIAMIA 101.


Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imekusanya na kuvuka lengo la ukusanyaji wa mapato mwezi Machi 2016 kwa asilimia 101. Lengo hilo limevukwa baada ya TRA kukusanya shilingi trilioni 1.31 kati ya lengo la shilingi trilioni 1.30, huu ni mwendelezo wa kuvuka malengo tangu Awamu ya Tano iingie madarakani.
Akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar es salaam leo kuhusu mwenendo wa makusanyo ya mapato, Kamishna Mkuu wa TRA Alphayo Kidata amesema ongezeko la makusanyo linatokana na jitihada zinazofanywa na TRA katika kuongeza kasi ya usimamizi wa ufuatiliaji na ukadiriaji wa kodi kwa usahihi.
“Tumejitahidi kudhibiti biashara za magendo katika maeneo ya Ukanda wa Pwani wa Bahari ya Hindi, mipakani na maziwa yote, Alisema Kamishna Mkuu.
Amesema hadi kufikia Machi 2016, tayari TRA imekusanya shilingi Trilioni 9.89 sawa na asilimia 99 ya lengo la makusanyo ya shilingi trilioni 9.99 ya lengo la miezi tisa.
Bw. Kidata amewasisitiza wafanyabiashara ambao hawajasajili biashara zao kufanya hivyo mara moja kupitia ofisi za TRA zilizoko katika maeneo ya biashara zao na kwa wale wanaoshiriki vitendo vya uingizaji bidhaa za magendo nchini amemewata kuacha mara moja kwani vinaipotezea serikali mapato.
“Wakikamatwa katika msako unaoendelea watachukuliwa hatua za kisheria ikiwemo kutaifisha bidhaa hizo, kutozwa faini pamoja na kifungo”, amesisitiza. Kwa Wafanyabiashara ambao wanastahili kupatiwa Namba ya Utambulisho wa Mlipakodi (TIN) Kamishna Mkuu amewataka kujisajili katika ofisi yoyote ya TRA na wahakikishe wana taarifa muhimu ikiwemo anuani inayotambulika na namba simu zinazofanya kazi.
“Natoa wito kwa wafanyabiashara wote waliosajiliwa na VAT lakini hawatumii mashine za kielektroniki za kodi (EFDs) watumie mashine hizo kwa mujibu wa sheria. Wakibainika hawazitumii watachukuliwa hatua za kisheria kwani zoezi la ukaguzi wa biashara linaendelea mtaa kwa mtaa katika mikoa yote. Aidha wananchi wanakumbushwa kudai risiti za kodi kwa thamani halisi ya manunuzi kila wanapofanya manunuzi au kupata huduma”, alisema Kamishna Mkuu na kuongeza kuwa wananchi wema na wazalendo wenye taarifa za ukwepaji wa kodi wazifikishe TRA kwa usiri. TRA inawaahidi donge nono ikiwa ni pamoja na kutunza siri za taarifa hizo. Vilevile wanapoadaiwa rushwa au kutendewa isivyo wasisite kutoa taarifa mara moja.
Imetolewa na:
Idara ya Huduma na Elimu kwa Mlipakodi
TRA- Makao Makuu

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni