Serikali imeagiza Maafisa Habari,Utamaduni ,Sanaa na Michezo Mikoani kuanza kushirikishwa katika vikao vya maamuzi ili wapate kujua mikakati ya maendeleo kwa sekta zao.
Agizo hilo limetolewa na Mheshimiwa Naibu Waziri wa Habari,Utamaduni Sanaa na Michezo Annastazia Wambura alipokuwa katika ziara ya kikazi Jijini Tanga kwa ambapo lengo la ziara hiyo ilikuwa ni kufuatilia utekelezaji wa shughuli za kisekta kwa Wizara yake katika Mkoa huo.

Mheshiwa Naibu Waziri Wambura alisema kushirikishwa katika vikao vya maamuzi kwa watendaji wa Kada hizo kutasaidia kuongeza chachu ya ukua wa sekta hizo katika mikoa pamoja na kutoa maoni ya kitaalum kwa sekta hizo kutoka kwao.
“Katika bajeti ya mwaka wa fedha 2017/2018 mtenge bajeti ya Kitengo cha Habari na pia mfanye utaratibu wa kupata Maafisa Habari kwa kuanzia ngazi ya Mkoa,Wilaya ,Halmashauri,pamoja na Jiji kwani kada hii ni muhimu kuwepo kwa lengo lakusaidia kutangaza maendeleo na fursa zilizopo katika Mkoa wenu,” alisema Mhe .Wambura.
Pamoja na hayo Mhe. Naibu Waziri Wambura aliendelea kusema Serikali inataka wananchi wapate kujua shughuli zote za maendeleo katika Mkoa wao zinafanyika vipi na mikakati ya maendeleo iko vipo,hivyo ni muhimu kupata Maafisa Habari watakao wasaidia kufanikisha hilo kazi ya kutoa habari hizo kwa umma.
Aidha, Naibu Waziri huyo alisisitiza kuwa Wizara kwa sasa ipo katika mazungumzo na TAMISEMI kwa jili ya kubadili mfumo na kuanzisha Kurugenzi za kisekta kwa Maafisa Habari,Maafisa Utamaduni,Maafisa Sanaa na Maafisa Michezo katika ngazi za Mikoa lengo ikiwa ni kuimarisha sekta hizo.
Kwa upande wa Mkuu wa Mkoa wa Tanga Bw. Martin Shigela alisema Mkoa huo unakabiliwa pia na uhaba wa Maafisa Michezo ,Maafisa Utamaduni na Maafisa Sanaa katika Mkoa na Halmashauri lakini suala hilo tayari wameanza kulifanyia kazi kwa kufanya utaratibu wa kupata Maafisa hao.
Halikadhalika naye Mkuu wa Wilaya ya Tanga Mjini Bw. Thobias Mwilapwa alimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa ziara yake kwa kuwa ametoa somo zuri la utendaji na pia anaamini atafanyia kazi kilio cha wadau wa michezo wa mkoa huo kwani ni mmoja wapo katika historia ya Michezo ,pamoja na Muziki wa Mwambao (Taarabu) pamoja na Mchezo wa Mbio za Baiskeli.
Pamoja na hayo naibu waziri huyo alitoa wito kwa wakazi wa Tanga katika kipindi wanapokuwa wakifanya shughuli za kimila na desturi kama za Jando na Unyago basi wawashirikishe wataalam wa Afya pamoja na wa Elimu kwa lengo la kutoa elimu ya afya ya uzazi halikadhalika kuelezewa umuhimu wa elimu katika maisha ya vijana wanaofanyiwa shughuli hizo.
Hata hivyo wakazi wote wa mkoa wa Tanga wametakiwa kuongeza juhudi za kusimamia muenendo mzuri wa maadili ya kitanzania ikiwa ni jukumu la kila mtu pamoja na kufanya kazi kwa kujituma zaidi kama kauli mbiu ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya HAPAKAZI TU!