Kikosi cha Mbeya City Fc tayari kimetua mkoani Shinyanga tayari kwa mchezo wa duru ya lala salama ya ligi kuu ya Vodacom Tanzania bara dhidi ya wenyeji Mwadui Fc, mchezo uliopangwa kuchezwa jumapili hii kwenye uwanja wa Mwadui uliopo nje kidogo ya mji huu wa kanda ya ziwa.
Afisa habari na mawasiliano wa kikosi cha City, Dismas Ten amesema leo asubuhi kuwa nyota wote 18 waliosafiri kwa ajili ya mchezo huo wako kwenye hali nzuri kiafya na kinachosubiriwa ni dakika 90 za siku ya mchezo.
“Tumekuja hapa na wachezaji 18,wote wako kwenye hali nzuri kwa mujibu wa daktari wetu, asubuhi hii tumefanya mazoezi mepesi na sasa tunasubiri siku ya mchezo,tunafahamu wapinzani wetu wana timu nzuri na pia wanacheza nyumbani, hilo halitupi shaka sana kwa sababu tuna kikosi ambacho kinaweza kushind popote, tumejiandaa vizuri na hilo ndiyo lengo letu”, alisema.
Kuhusu wachezaji waliosafiri kutoka jijini Mbeya kwa ajili ya mchezo huo Ten alisema kuwa City imelazimika kumuondoa kikosini mlinzi Hassan Mwasapili kutokana na kuwa na kadi tatu za njano hivyo hawezi kuwa sehemu ya mchezo huo.
“Tumemuacha Mwasapili hii ni kwa sababu ana kadi tatu za njano,kwa vyovyote tusingeweza kumtumia, badala yake tumesafiri na Yusuph Abdalah mbaye amekuwa kwenye kiwango kizuri mazoezini hasa baada ya kupona majeraha” alisema Ten, huku akiwataja nyota wengine walio kwenye msafara huo kuwa ni pamoja na;
Juma Kaseja, Hanningtony Kalyesubula, John Kabanda, John Jerome, Yusuph Abdalah, Yohana Moriss, Tumba Sued, Haruna Shamte, Kenny Ally,Ramadhan Chombo, Raphael Daud, Geoffrey Mlawa, Salvatory Nkulula, Joseph Mahundi na wengine.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni